Mwalimu Msaidizi wa Shule ya Msingi Kivule ya Manispaa ya Ilala, Wilson
Muhemba akionyesha ubao ulioandikwa gharama za uchangiaji wa mtoto
anayeingia darasa la kwanza jana.
Picha na Pamela Chologola.
Dar/Moro/Mbeya. Msimu wa
uandikishaji watoto wanaoanza darasa la kwanza, umeanza, huku kukiwa na
malalamiko lukuki hasa kutokana na michango inayotozwa kwa watoto
wanaokwenda kuanza darasa la kwanza.
Itakumbukwa, Novemba 7, 2012, Naibu Waziri katika
Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
anayeshughulikia Elimu, Majaliwa Kassim Majaliwa alisema bungeni mjini
Dodoma kuwa ni kosa kwa walimu wakuu kutoza fedha kwa watoto wanaoanza
darasa la kwanza na atakayefanya hivyo atachukuliwa hatua kali za
kisheria.
Majaliwa alikuwa akibu swali la nyongeza la Mbunge
wa Kawe (Chadema), Halima Mdee, alisema kama ni michango ni ile
iliyokubaliwa na wazazi wenyewe, Kamati za Shule lakini pia na kupata
baraka za mamlaka husika za elimu katika Halmashauri au Wilaya.
Hata hivyo, kauli hiyo ya Serikali, inaonekana
kupigwa kumbo huku wazazi wakishangaa michango hiyo, ambayo mingine
haieleweki na mingine ilikubalika kupitia kamati za shule.
Tozo la kujiandikisha:
Wazazi wa watoto waliokwenda kujiandikisha katika
Shule ya Msingi Kivule wameulalamikia uongozi wa shule hiyo kuwachagisha
kiasi cha Sh40,000 kwa ajili ya watoto wanaojiunga darasa la kwanza
jambo lililosababisha watoto kushindwa kujiunga.
Malalamiko kama hayo ambayo yako kwenye shule
mbalimbali, pia yaliibuka katika Shule ya Msingi Mtoni, Dar es Salaam
kwa wazazi kulalamikia kutozwa Sh33,500 wakati mjini Morogoro katika
Shule ya Msingi Kambarage iliyopo Kata ya Chamwino katika Manispaa ya
Morogoro michango ilifikia Sh50,000 kwa kila mzazi.
Katika Shule ya Msingi Kivule, Dar es Salaam,
wazazi wameulalamikia uongozi kukataa kuwaandikisha watoto na wazazi
kulazimishwa kutoa Sh40,000 ndipo watoto wao waandikishwe kuanza darasa
la kwanza mwaka huu.
Mwandishi wa habari hizi alipomtafuta Mwalimu Mkuu
Msaidizi wa shule hiyo, Wilson Muhemba, alikana madai hayo na kusema
anachoelewa yeye ni mchango wa Sh15,000 kwa ajili ya kujenga madarasa ya
shule mpya ambayo ilipitishwa kwenye kikao cha wazazi.
Mmoja wa wazazi aliyejitambulisha; Rozi Mwing’a
alisema alifika shuleni hapo kwa ajili ya kuwaandikisha watoto wake
wawili aliambiwa atoe mchango wa Sh40,000 kwa kila mtoto hivyo
imesababishia kushindwa kuwaandikisha watoto hao.
Alisema wanachangia michango wa ujenzi wa shule
Sh15,000, mchango wa fulana Sh6,000, mchango wa mafunzo ya awali
Sh6,000, nembo Sh1,000 na ulinzi ni Sh5,000.
Mwing’a alisema mchango mwingine wa fomu Sh5,000,
kupima uzito Sh1,000, picha za pasipoti Sh3000 na mchango wa madaftari
saba Sh1,500.
Na Waandishi Wetu, Mwananchi
Na Waandishi Wetu, Mwananchi
0 comments:
Post a Comment