Jumla ya 
Walimu wapya 36,021 ambao wamehitimu mwaka 2013 kutoka vyuo mbalimbali 
hapa nchini wataajiriwa rasmi na Mamlaka za Serikali za Mitaa 
(Halmashauri) ifikapo tarehe 01 Aprili 2014. Kati ya idadi hiyo walimu 
wa ngazi ya Cheti (Daraja III A) ambao hufundisha katika shule za Msingi
 ni 17,928 na walimu wa shule za sekondari ni 18,093 (wakiwemo 5,416 wa 
Stashahada na 12,677 wenye shahada).
Orodha rasmi ya walimu wapya ikionesha
 Halmashauri mbalimbali walikopangwa itatangazwa kwenye tovuti ya Ofisi 
ya Waziri Mkuu TAMISEMI (www.pmoralg.go.tz) na ya Wizara ya Elimu na 
Mafunzo ya Ufundi (www.moe.go.tz) ifikapo tarehe 15 Machi, 2014.
Walimu wote wapya wanatakiwa kuripoti 
bila kukosa kwenye Halmashauri walikopangiwa ifikapo tarehe 01 Aprili, 
2014 ili waanze kazi mara moja.
Inasisitizwa kwamba walimu waripoti 
tarehe hiyo ili taarifa zao za kiutumishi zifanyiwe kazi na Waajiri wao 
yaani Wakurugenzi ili kuwawezesha kupata mshahara mwezi Aprili 2014 na 
hivyo kuepuka ulimbikizaji wa mshahara kwa watumishi wapya wanaoanza 
ajira.
Mwalimu yoyote ambaye ataripoti baada 
ya tarehe 10 Aprili, 2014 bila sababu za msingi zinazokubalika 
kiutumishi atakuwa amepoteza nafasi hiyo.
Ikumbukwe kwamba Upangaji wa Walimu 
wapya kwenye Halmashauri umezingatia uwepo wa mahitaji ya walimu. Vile 
vile, fedha za kujikimu kwa muda wa siku saba na nauli ambazo zitalipwa 
kwa kila mwalimu atakayeripoti kulingana na viwango vilivyowekwa na 
Serikali zimetumwa kwenye Halmashauri walikopangwa walimu hao. Hivyo, 
kila mwalimu anatakiwa kwenda kuripoti katika Halmashauri alikopangwa.
Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI 
haitafanya mabadiliko yoyote ya vituo vya kufanya kazi walimu wapya 
isipokuwa kwa utaratibu wa kawaida wa uhamisho baada ya mwalimu kutimiza
 vigezo na masharti ya uhamisho.
Ni vema ifahamike kuwa ajira 
zinazotangazwa ni za walimu wapya. Walimu ambao tayari ni watumishi umma
 waliokuwa vyuoni kwa ajili ya kujiendeleza kielimu na hivi sasa 
wamehitimu mafunzo yao, wanatakiwa kurudi kwa waajiri wao na kuendelea 
na kazi.
Ofisi ya waziri mkuu- TAMISEMI.
 






 
 
 
 






0 comments:
Post a Comment