Wednesday, 22 January 2014

WAFUNGWA WATOROKA GEREZANI MKOANI MBEYA BAADA YA KUKATA NONDO KWA MSUMENO

*Wadaiwa kukata nondo za gereza na msumeno

WAFUNGWA watatu wa gereza la Songwe wilaya ya Mbeya Vijijini mkoani hapa, wametoroka katika mazingira yenye utata wakiwa ndani ya sero ya gereza hilo.

Tukio hilo la kushangaza, lilitokea kati ya Januari 14 na 15, mwaka huu, ambapo wafungwa hao inadaiwa kuwa walikata nondo za dirisha la sero walimokuwemo kisha kuruka na kutokomea kusikojulikana.

Taarifa za uchunguzi, zimebaini kuwa, wafungwa hao walikata nondo hizo kwa kutumia msumeno bila kubainika na askari waliokuwa kazini siku hiyo.

Taarifa zinasema kuwa, wafungwa hao ni wakazi wa wilaya za Mbeya na Chunya ambapo mmoja wao alikutana na Kamanda wa polisi wa wilaya ya Chunya, alipoulizwa kuwa ametokaje gerezani, alimwambia kamanda huyo kuwa alitoka kwa msamaha wa Rais.

Mkuu wa magereza mkoa wa Mbeya SACP, Julius Sanguti,  amethibitisha kutoroka kwa wafungwa hao.

“Ni kweli lakini ni mapema mno kulizungumzia tukio hilo kwasababu tunaendelea na uchunguzi kwa kushirikiana na wenzetu wa jeshi la Polisi’’ alisema Sanguti.

Alipoulizwa kama kuna askari anashikiliwa kwa uzembe na kama ana taarifa waliko wafungwa hao, alisema hakuna mtu yeyote anayeshikiliwa kwa sasa kwasababu wanafanya uchunguzi.

‘’Ndiyo maana nimekuambia kuwa ni mapema mno na tukimaliza uchunguzi au tukiwakamata nitasema’’ alisema SACP Sanguti.

Alipotafutwa kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi, simu yake alipokea (Bodyguard) wake na kusema kuwa kamanda huyo alikuwa msibani.

Mbali na tukio hilo katika gereza la Songwe, pia taarifa zinasema kuwa katika gereza la Ruanda hivi karibuni, alitoroka mahabusu mwenye asili yaEthiopia lakini tayari amekamatwa.

Related Posts:

0 comments: