Wednesday 30 April 2014

BILA UWEKEZAJI TUNAJIDANGANYA – WAZIRI MKUU

 1(5) 
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amesema bila uwekezaji nchi haiwezi kusonga mbele na akawataka watendaji serikalini kubadili mtazamowao kuhusiana na suala zima la uwekezaji.
Ametoa kauli hiyo jana usiku (Jumanne, Aprili 29, 2014) wakati akizungumza na wafanyabiashara na wajasiriamali mbalimbali wa hapa nchini kwenye hafla fupi ya uzinduzi wa Taasisi ya Mkoba Private Equity Fund inayojishughulisha na utoaji mitaji kwa wajasiriamali wadogo na wa kati. “Bila uwekezaji tunajidanganya… ni ukweli usiopingika kwamba uwekezaji mkubwa unatoka kwenye sekta binafsi, kwa hiyo watendaji wetu serikalini wanapaswa kubadili mtazamo wanaposhughulikia masuala ya sekta binafsi,” alisema.
Alisema watendaji serikalini wanapaswa kubadili mitazamo yao hasa wanapokuwa wanawasiliana na watu wa sekta binafsi kwa sababu kwa mfanyabiashara yeyote wakati ni mali.
“Tanzania imejipanga kuelekea kuwa Taifa lenye uchumi wa kati, kama kweli tunataka kufika huko mapema ni lazima tuwachukulie wadau wa sekta kwa mtazamo wa tofauti. Siyo anakuja kutaka taarifa unaanza kumzungusha bila sababu, anataka kusajili kampuni unamwambia unajua mafaili hayaonekani wakati hakuna cha mafaili wala nini bali unatafuta mwanya wa kudai chochote,” alisema.
Akizungumzia kuhusu utoaji mikopo kwa ajili ya mitaji ya kibiashara, Waziri Mkuu aliitaka Taasisi ya Mkoba Equity Fund ihakikishe inajenga kwanza uwezo wa wahusika ili waweze kuzalisha mali kama ilivyokusudiwa.
Akitoa mfano wake binafsi, Waziri Mkuu alisema wakati anaanza biashara ya ufugaji nyuki miaka mitatu iliyopita, hakuwahi kuandaa mchanganuo wowote (write-up) wala hakuwahi kuandaa mpango wa biashara (business plan). Matokeo yake, alikuwa anatoa tu fedha mfukoni na kununua vifaa kadri mahitaji yalivyokuwa yakijitokeza, jambo ambalo alisema si sahihi.
“Ninawasihi sana viongozi wa Mkoba Equity Fund wasitoe mikopo kwa watu wanaotaka kufanya biashara kama nilivyoanza mimi. Wekezeni kwanza kwa kuwajengea uwezo wajasiriamali watakaoomba fedha za mitaji kutoka kwenye taasisi hii,” alisisitiza.
Akitoa ushauri kwa wajasiriamali wadogo waliotoa shuhuda zao kuhusu changamoto walizokabiliana nazo wakati wakianzisha biashara zao, Waziri Mkuu aliwataka wasirudi nyuma wala wasikate tamaa. “Fursa ni nyingi sana na mnaweza kufanya mambo mengi. Kitu cha msingi ni kuwa na nia thabiti (determination).
Wajasiriamali walitoa shuhuda zao ni Mkurugenzi wa kampuni ya Montage, Bi. Teddy Mapunda; Mkurugenzi wa kampuni ya Go-Financing, Bw. Geoffrey Ndossi, Mkurugenzi wa kampuni ya SIGA Ltd, Bw. Marwa Busigara na Mkurugenzi wa kampuni ya WIA, Bw. Eric Mwenda.

0 comments: