Sunday 16 June 2013

SIMBA NA YANGA KUPEWA BULLET PROOF KATIKA KOMBE LA KAGAME




WACHEZAJI na viongozi wa timu zitakazoshiriki michuano ya Kombe la Kagame zikiwemo Simba, Yanga na Falcon nchini Sudan, watalazimika kuvaa fulana zisizopitisha risasi kwa ajili ya usalama.
 https://sphotos-b.xx.fbcdn.net/hphotos-frc3/p480x480/261610_638194326193930_1095712542_n.jpg
Hayo yamesemwa jana na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Amos Makalla wakati akitoa msimamo mpya wa serikali juu ya ushiriki wa timu za Tanzania katika michuano hiyo.

Awali, Simba, Yanga na Falcon zilikuwa kwenye uwezekano wa kutoshiriki kwa sababu za kiusalana hasa katika Jimbo la Darfur ambalo ni kiini cha machafuko nchini humo.

Makalla alisema baada ya Serikali ya Sudan kuihakikishia Tanzania usalama, timu hizo zitashiriki lakini wachezaji na viongozi wake watavalia fulana hizo zisizopitisha risasi.

Makalla alisema jana kuwa Serikali ya Sudan pia imethibitisha kwa barua kwamba itawapokea wachezaji hao kuanzia Khartoum ambako timu hizo zitafikia na kuwasafirisha kwa basi hadi miji ya Darfur na Kordofan.

Uamuzi huo unakuja siku nne tu, tangu Makalla alitangazie Bunge kuwa, Tanzania haitapeleka timu zake katika nchi hiyo kutokana na usalama mdogo, wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Sumve, Richard Ndassa (CCM).

Makalla alisema jana, awali walichukua msimamo huo wa kutokana na kutokuwa na uthibitisho kutoka kwa nchi husika, badala yake Baraza la Vyama vya Soka Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), ndilo limekuwa likitoa taarifa.

“Kwa taarifa tulizozipata, mazingira ya kule hayakuwa salama na tulimtaka Leodegar Tenga ambaye ni Mwenyekiti wa Cecafa, yeye kama Mtanzania mwenzetu, suala hili anabebaje dhamana na pia tukamtaka atueleze, kwanini tunapata uthibitisho kutoka CECAFA badala ya serikali. Hatimaye sasa serikali yenyewe ndiyo imetuandikia barua,” alisema.

Juni 1, Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe wakati akihitimisha hotuba ya bajeti ya wizara yake, alisema anashangaa kuona Darfur ikipewa uenyeji wa michuano hiyo licha ya kuwa na usalama mdogo.

Alisema kwa mujibu wa sheria za kimataifa kwenye nchi zenye machafuko ili michuano kama hiyo iweze kufanyika ni lazima sehemu husika wanakofikia wachezaji na maofisa wengine, kuwe na magari maalumu ya kuzuia risasi (bullet proof) ya kuwabeba kutoka uwanja wa ndege hadi sehemu wanakokwenda.

Membe alisema wachezaji na viongozi wengine watakaokwenda Darfur, wanapaswa kupewa fulana maalumu za kuzuia risasi, ambazo watapaswa kuzivaa wakati wote kwa ajili ya usalama wao.

Aliongeza kuwa mbali ya matatizo ya kiusalama, pia mji wa Darfur hauna hoteli zenye uwezo wa kuwatosheleza wageni wote watakaokwenda kwa ajili ya michuano hiyo.

Waziri Membe alihoji busara gani iliyotumiwa na CECAFA kuteua nchi hiyo kuwa mwenyeji wa michuano hiyo inayotarajiwa kuanza Juni 18.

Wakati Yanga ikishiriki michuano hiyo kama bingwa mtetezi, Simba imejitwalia tiketi ya moja kwa moja kama mabingwa wa msimu uliopita, kama ilivyo kwa Falcon, ambayo licha ya kushuka daraja msimu huu, itashiriki michuano hiyo.

Tangu mwaka 2002, michuano hiyo imekuwa ikifanyika chini ya udhamini wa Rais wa Rwanda, Paul Kagame, ambaye hutoa zawadi kwa mshindi wa kwanza hadi wa tatu.

0 comments: