Amri hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mfawidhi, Isaya Arufani, kwa ajili ya usalama wa mashahidi hao wa upande wa Jamhuri.
Hata hivyo shahidi wa pili wa upande 
wa Jamhuri, alidai washitakiwa hao ambao ni Huang Gin, Xu Fujie na Chen 
Jinzha, walitoa hongo ya Sh milioni 30.2 kwa polisi na askari wa Wanyama
 Pori ili wasipekue nyumba waliyokuwa wakiishi iliyopo mtaa wa Kifaru, 
Mikocheni Dar es Salaam.
Wanadaiwa walikutwa na nyara za 
Serikali, ambazo ni vipande 706 vya meno ya tembo vyenye uzito wa 
kilogramu 1,880, vyote vikiwa na thamani ya Sh bilioni 5.4.
Shahidi huyo alidai wakati wakiendelea
 kufanya upekuzi kwenye nyumba waliyokuwa wakiishi washtakiwa hao, 
mshtakiwa Huang Gin alivuta droo na kutoa bahasha iliyokuwa na fedha 
ndani, ambazo walipozihesabu zilikuwa ni Sh milioni 30.2, kama 
kishawishi cha kuwataka wasiendelee kuipekua nyumba hiyo.
“Tuliendelea kufanya upekuzi kwenye 
nyumba hiyo, tukakuta kuna makontena yamepangwa chini manne, juu yake 
matatu, tuliyafanyia upekuzi na mojawapo lilikuwa na vipande 706 vya 
meno ya tembo ambayo yalikuwa yamehifadhiwa kwenye mifuko ya viroba 54,”
 aliieleza Mahakama.
Aliongeza kudai kuwa mbali na meno 
hayo ya tembo, pia walikamata mizani tatu, kompyuta mpakato na magari 
matatu, yaliyokuwa yakihusishwa kutumika kwenye biashara hiyo haramu.
Shahidi huyo aliieleza Mahakama kuwa 
wakati yote hayo yakiendelea mshtakiwa wa kwanza na wa pili, walikuwa 
wakizungumza Kiswahili huku mshtakiwa wa tatu alikuwa akizungumza 
Kiingereza.
Alidai baada ya kuwaweka washtakiwa 
hao chini ya ulinzi na kuwapeleka katika kituo cha Polisi cha Oysterbay 
kwa ajili ya mahojiano, walibadilika na kuwa hawawezi kuongea Kiswahili 
wala Kiingereza, kitu ambacho kiliwalazimu kumtafuta mkalimani.
Walimtafuta mkalimani, wakahojiwa na 
hatimaye wakafunguliwa mashtaka yanayowakabili na kwamba meno hayo ya 
tembo yamehifadhiwa kwenye ghala la Hifadhi ya Taifa ya Meno ya Tembo.
Kukamatwa kwa washtakiwa hao ni baada 
ya timu ya shahidi huyo ya polisi, akishirikiana na askari kutoka Idara 
ya Wanyama Pori kupata taarifa ya siri, iliyowaeleza kuwa kuna raia 
watatu wa China, wanajihusisha na biashara haramu ya meno ya tembo na 
kwamba walikuwa wakitumia magari matatu kwa nyakati tofauti. CHANZO:HABARILE












0 comments:
Post a Comment