Wednesday, 5 March 2014

WAANDISHI WABANWA KESI YA WACHINA

kisutu5_6e3a1.jpg
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imetoa amri kwa vyombo vya habari, kutoandika majina ya mashahidi katika kesi ya kukutwa na meno ya tembo yenye thamani ya Sh bilion 5.4, inayowakabili raia watatu wa China.
Amri hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mfawidhi, Isaya Arufani, kwa ajili ya usalama wa mashahidi hao wa upande wa Jamhuri.
Hata hivyo shahidi wa pili wa upande wa Jamhuri, alidai washitakiwa hao ambao ni Huang Gin, Xu Fujie na Chen Jinzha, walitoa hongo ya Sh milioni 30.2 kwa polisi na askari wa Wanyama Pori ili wasipekue nyumba waliyokuwa wakiishi iliyopo mtaa wa Kifaru, Mikocheni Dar es Salaam.
Wanadaiwa walikutwa na nyara za Serikali, ambazo ni vipande 706 vya meno ya tembo vyenye uzito wa kilogramu 1,880, vyote vikiwa na thamani ya Sh bilioni 5.4.
Shahidi huyo alidai wakati wakiendelea kufanya upekuzi kwenye nyumba waliyokuwa wakiishi washtakiwa hao, mshtakiwa Huang Gin alivuta droo na kutoa bahasha iliyokuwa na fedha ndani, ambazo walipozihesabu zilikuwa ni Sh milioni 30.2, kama kishawishi cha kuwataka wasiendelee kuipekua nyumba hiyo.
“Tuliendelea kufanya upekuzi kwenye nyumba hiyo, tukakuta kuna makontena yamepangwa chini manne, juu yake matatu, tuliyafanyia upekuzi na mojawapo lilikuwa na vipande 706 vya meno ya tembo ambayo yalikuwa yamehifadhiwa kwenye mifuko ya viroba 54,” aliieleza Mahakama.
Aliongeza kudai kuwa mbali na meno hayo ya tembo, pia walikamata mizani tatu, kompyuta mpakato na magari matatu, yaliyokuwa yakihusishwa kutumika kwenye biashara hiyo haramu.
Shahidi huyo aliieleza Mahakama kuwa wakati yote hayo yakiendelea mshtakiwa wa kwanza na wa pili, walikuwa wakizungumza Kiswahili huku mshtakiwa wa tatu alikuwa akizungumza Kiingereza.
Alidai baada ya kuwaweka washtakiwa hao chini ya ulinzi na kuwapeleka katika kituo cha Polisi cha Oysterbay kwa ajili ya mahojiano, walibadilika na kuwa hawawezi kuongea Kiswahili wala Kiingereza, kitu ambacho kiliwalazimu kumtafuta mkalimani.
Walimtafuta mkalimani, wakahojiwa na hatimaye wakafunguliwa mashtaka yanayowakabili na kwamba meno hayo ya tembo yamehifadhiwa kwenye ghala la Hifadhi ya Taifa ya Meno ya Tembo.
Kukamatwa kwa washtakiwa hao ni baada ya timu ya shahidi huyo ya polisi, akishirikiana na askari kutoka Idara ya Wanyama Pori kupata taarifa ya siri, iliyowaeleza kuwa kuna raia watatu wa China, wanajihusisha na biashara haramu ya meno ya tembo na kwamba walikuwa wakitumia magari matatu kwa nyakati tofauti
CHANZO:HABARILE

0 comments: