Na James Magai, Mwananchi
Dar es Salaam. Katibu wa Jumuiya na 
Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Issa Ponda leo anatarajiwa kuwa na 
kibarua kingine kigumu katika kupangua kigingi cha kufutiwa shtaka la 
kukaidi amri ya mahakama, alichowekewa na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP).
Sheikh Ponda kwa sasa anasota mahabusu
 kutokana na kesi ya jinai inayomkabili katika Mahakama ya Hakimu Mkazi 
Morogoro, akidaiwa kufanya makosa ya uchochezi katika maeneo mbalimbali 
mjini Morogoro na kukiuka amri ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu
.
Hata hivyo Ponda kupitia kwa Wakili 
wake Juma Nassoro, amewasilisha maombi ya marejeo, akiiomba Mahakama Kuu
 ifanye marejeo ya uamuzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro kukataa 
maombi yake ya kumfutia shtaka hilo.
Maombi hayo yalitarajiwa kusikilizwa 
na Jaji Agustine Mwarija juma lililopita lakini yaligonga mwamba baada 
ya DPP kuwasilisha pingamizi mahakamani hapo akiiomba mahakama 
iyatupilie mbali maombi hayo, pamoja na mambo mengine akidai kuwa, 
yamewasilishwa kinyume cha sheria.
Kutokana na pingamizi hilo, Jaji 
Mwarija aliahirisha usikilizwaji wa maombi hayo ya msingi hadi leo kwa 
ajili ya kusikiliza pingamizi hilo la DPP.
Katika pingamizi hilo, DPP kupitia kwa
 Wakili wa Serikali, Bernard Kongola alidai kuwa maombi hayo 
yamewasilishwa kinyume na kifungu cha 372 (2) Sheria ya Mwenendo wa 
Makosa ya Jinai (CPA).
Alidai kwa mujibu wa kifungu hicho mtu
 haruhusiwi kuwasilisha ombi la marejeo ambayo yanatokana na uamuzi au 
amri ya mahakama ya chini ambayo haimalizi kesi.
Hii ni mara ya pili kwa Sheikh Ponda 
kuwasilisha mahakamani hapo maombi hayo baada ya Mahakama Kuu 
kuyatupilia mbali kutokana na pingamizi lililowekwa na DPP.
Maombi hayo ya kwanza yalitupiliwa 
mbali na Jaji Rose Teemba,Desemba 11, 2013, baada ya DPP kumwekea 
pingamizi kuwa hati ya kiapo iliyokuwa ikiunga mkono maombi yake ilikuwa
 na kasoro za kisheria












0 comments:
Post a Comment