Monday, 3 March 2014

CCM WATOA RAMBIRAMBI MIL. 1/-, CHADEMA YATOA 50,OOO/-


 ccm_9756b.jpg
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimetoa Sh milioni moja kwa familia tatu zilizofiwa na ndugu zao katika ajali mbaya ya gari, iliyotokea Februari 27, katika mlima wa Ipwasu, jimbo la Kalenga, Iringa Vijijini.
Kwa upande wao Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), nacho kimejipigapiga na kutoa Sh 50,000 kwa familia hizo.
Msiba huo umetokea huku vyama hivyo vikiwa katika harakati za kuomba kura kwa wapiga kura 85,051 wa jimbo hilo katika uchaguzi mdogo wa ubunge, utakaofanyika Machi 16 baada ya aliyekuwa mbunge wake, Dk William Mgimwa kufariki dunia.
Kwa upande wake, CCM imemsimamisha Godfrey Mgimwa (32) wakati Grace Tendega anagombea kupitia Chadema. Chama kingine kinachoshiriki uchaguzi huo ni Chausta, kilichomsimamisha Richard Minja, ambaye hana ratiba ya kampeni jimboni humo hadi sasa.
Katika ajali hiyo, iliyohusisha gari la mizigo aina ya Fuso lenye namba za usajili T250 AFJ, Hanskari Chengulla, Sabasaba Kiseve na Nyagile Luvanda, walikufa papo hapo.
Lori hilo mali ya Kiwanda cha Maji Afrika, lililokuwa likiendeshwa na Luvanda, lilikuwa likipeleka maji ya chupa katika kijiji cha Tangamalenga.
Mgombea wa CCM, Mgimwa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Mwigulu Nchemba walikuwa kivutio wakati mamia ya waombolezaji wakishiriki mazishi ya vijana hao.
Baada ya miili ya marehemu kuhifadhiwa katika nyumba zake za milele, Chadema walikuwa wa kwanza kupewa fursa ya kutoa rambirambi zao.
Katika salamu zao, Chadema waliahidi kuchangia Sh 50,000 huku wakiahidi kuwa pamoja na familia za waliopoteza maisha yao katika ajali hiyo.
Baada ya kutoa rambirambi ya Sh milioni moja kwa niaba ya chama chake, Nchemba alisema CCM imeguswa na vifo vya vijana hao, waliokuwa wakitegemewa na familia zao pamoja na maendeleo ya Taifa.
Alisema CCM iko pamoja na familia za marehemu katika kipindi hicho kigumu na alimuagiza mgombea ubunge katika jimbo hilo, kuzikumbuka familia hizo kwa kusaidia kusomesha watoto walioachwa na marehemu hao.
“Mgimwa, haya ndio majukumu ya kisiasa, huu ni sehemu ya mzigo wako, ukishinda uchaguzi moja ya kazi unayotakiwa kufanya ni kusaidia kusomesha watoto wa ndugu zetu hawa waliotutoka,” alisema.
CHANZO:HABARILEO

Related Posts:

0 comments: