Monday 26 May 2014

STARS YAWASILI KESHO DAR KUIVAA MALAWI TAIFA

Na Boniface Wambura, DAR ES SALAAM KIKOSI cha timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars kilichopiga kambi Tukuyu mkoani Mbeya, kitawasili mjini Dar es Salaam kesho Saa 4:00 asubuhi kwa ndege ya Air Tanzania tayari kwa mchezo wa kirafiki na Malawi. Taifa Stars na Malawi ‘Flames’ zitapambana kesho katika mechi ya kirafiki ya kimataifa itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 11:00 jioni. Malawi tayari ipo mjini Dar es Salaam kwa ajili ya mechi hiyo na imefikia katika hoteli ya Sapphire Court, Kariakoo.
Stars itawasili kesho Dar es Salaam ikitokea Mbeya kwa ajili ya mchezo na Malawi kesho hiyo hiyo jioni
Kiingilio katika mechi hiyo kitakuwa sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, bluu na kijani. Kwa upande wa VIP B na C kiingilio kitakuwa sh. 10,000 wakati kwa VIP A itakuwa ni sh. 20,000. Hiyo itakuwa ni mechi ya mwisho ya majaribio kwa Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager kabla ya kwenda jijini Harare kwa ajili ya mechi ya marudiano ya michuano ya Afrika dhidi ya Zimbabwe (Mighty Warriors). Malawi (Flames) inayonolewa na mchezaji wake wa zamani Young Chidmozi nayo itakuwa inacheza mechi ya mwisho ya majaribio kabla ya kwenda N’djamena kuikabili Chad.

0 comments: