Felix Mwagara
SERIKALI
 imewapa uraia wa Tanzania Wakimbizi wa Kisomali wenye asili ya Kibantu 
1,514 waliokuwa wanaishi katika Makazi ya Chogo, Wilaya ya Handeni 
mkoani Tanga. 
Wakimbizi
 hao ambao walikimbia nchi yao Somalia baada ya vita kutokea mwaka 1990 
ambapo baadhi yao 3,000 walikimbilia nchini kwa kutambua kuwa ndipo 
mababu zao walikotoka, Serikali iliwapokea na kuwahifadhi katika Kambi 
ya Mkuyu iliyopo Mkoani Tanga ambapo walikuwa wakipata msaada kutoka 
Shirika la Kuhudumia Wakimbizi Duniani (UNHCR).
Akizungumza
 jana baada ya kuwapa vyeti vya uraia wakimbizi hao ambao kwasasa ni 
raia halali wa Tanzania, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias 
Chikawe alisema wakimbizi hao walihamishwa na Serikali mwaka 2003 kutoka
 Kambi ya Mkuyu kuja katika Makazi ya Chogo ili wapatiwe mashamba kwa 
ajili ya kujishughulisha na kilimo ili waweze kujitegemea.
“Nachukua
 nafasi hii kuwapongeza wote waliopewa uraia wa Tanzania, wajisikie kuwa
 wao ni raia huru sawa na Watanzania wengine. Hata hivyo nawasihi muwe 
waadilifu na watiifu kwa sheria zote za Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania,” alisema Chikawe.
Chikawe
 pia alitoa pongezi kwa UNHCR kwa kujenga miundombinu muhimu katika 
makazi hayo ya Chogo na pia kuwawezesha wakimbizi hao kuishi maisha ya 
kujitegemea wenyewe kabla hata ya kuwa raia.
Hata
 hivyo, Waziri Chikawe aliwataka wakimbizi 150 katika makazi hayo ya 
Chogo ambao hawakuomba kuwa raia wa Tanzania kwa nia ya kurudi nchini 
Somalia pale hali ya amani itakapopatikana wanapaswa kuendelea kutii 
sheria za nchi zinazotawala hifadhi ya ukimbizi nchini.
Aidha,
 Mwakilishi Mkazi wa UNHCR, Joyce Mends-Cole katika hafla hiyo 
aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuwapa uraia wakimbizi hao na 
Shirika lake litaendelea kutoa misaada mbalimbali kwa wakimbizi 
waliobaki katika makazi hayo pamoja na sehemu nyingine nchini. 
Hafla
 hiyo ya ugawaji wa vyeti vya uraia ilihudhuriwa na Maofisa wa Idara ya 
Wakimbizi na Uhamiaji zilizopo Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, 
Mwakilishi wa Mkuuu wa Mkoa wa Tanga na Serikali ya Kijiji cha Chogo 
pamoja na Maofisa wa UNHCR
 






 
 
 
 






0 comments:
Post a Comment