Thursday, 3 July 2014

KOMBE LA DUNIA:NEYMAR FITI, HAZARD NA MBIU YA ‘KUMSIMAMISHA’ MESSI!!


>>SCOLARI AMWITA MWANASAIKOLOJIA KAMBINI KUSAIDIA WACHEZAJI!
BRAZIL Ijumaa na Jumamosi itashuhudia Mechi za Robo Fainali za Kombe la Dunia na hii ni kufa na kupona kwa Nchi 8 zinazogombea Nafasi 4 za Nusu Fainali lakini presha kubwa iko kwa Wenyeji Brazil ambao walipata kashikashi kubwa kuitoa Chile Raundi iliyopita kiasi cha baada ya Mechi Kocha wao Luiz Felipe Scolari kumwita Kambini Mwanasaikolojia lakini habari njema kwao ni kupona kwa Neymar wakati Kambi ya Belgium, ambayo itaikabili Argentina, mchecheto mkubwa ni kumzuia Lionel Messi kiasi cha Staa Eden Hazard kupiga mbiu.
SOMA ZAIDI: 
Neymar fiti kuikabili Colombia Robo Fainali
NEYMAR-BRAZIL-CAMEROONNeymar amesema yuko fiti kuikabili Colombia Ijumaa Usiku wakati Nchi yake Brazil itakapokutana na Colombia kwenye Robo Fainali ya Kombe la Dunia huko Fortaleza baada kuwepo wasiwasi mkubwa kwamba ana maumivu.
Kwenye Mechi iliyopita, Brazil walipoitoa Chile kwa Penati baada ya kutoka Sare 1-1 katika Dakika 120, mara mbili Neymar alilazimika kutoka nje kutibiwa baada kugongwa kwenye Goti na Pajani.
Neymar ndie aliefunga Penati iliyowapa ushindi Brazil lakini alimaliza Mechi hiyo akiwa na michubuko na uvimbe.
Akiongea baada ya kumaliza Mazoezi kwenye Kambi ya Brazil huko Teresópolis, Neymar alisema: “Nitaweza kucheza na Colombia. Sisikii maumivu. Nimekuwa nikifanya Mazoezi vizuri. Hamna wasiwasi.”
Luiz Felipe Scolari amwita Mwanasaikolojia Kambini
Bosi wa Brazil Luiz Felipe Scolari amemwita Mwanasaikolojia Kambini mwa Timu yake mara baada ya Mechi yao iliyopita waliyoitoa Chile kwa Penati baada ya kutoka Sare 1-1 katika Dakika 120.LUIZ_FELIPE_SCOLARI
Baada ya Mechi hiyo, Wachezaji kadhaa wa Brazil walionekana wakibubujikwa machozi walipokuwa wakisheherekea ushindi wao.
Mmoja wa Wachezaji hao alikuwa Neymar ambae amekiri Gemu hiyo na Chile iliwapa msisimko lakini amekataa kwamba Kikosi chao kimetingwa na mawazo.
Hata hivyo, hatua hii ya Scolari ya kumtumia Mwanasaikolojia ni mbinu dhahiri ya kuwapunguzia presha Wachezaji wake ambao wamebeba zigo zima la kuwa Wenyeji wa Kombe la Dunia wanaotakiwa kutwaa Kombe hilo.
Akijizungumzia binafsi, Neymar, ambae ndie anaonekana aliebeba zigo zito na ambae ameifungia Brazil Bao 4 hadi sasa, ameeleza: “Sijisikii mzigo wowote wa kuwekwa mbele. Ninao wenzangu kwenye Timu wanaonisaidia. Wengine hupokonya Mipira, wenginehutoa pasi, wengine hufunga. Sisi ni Timu!”
Hazard: ‘Lazima tumsimamishe Messi!’
EDEN_HAZARDMshambuliaji wa Belgium Eden Hazard amebainisha kwamba kumsimamisha Staa wa Argentina Lionel Messi kutaisaidia sana Timu yao kuifunga Argentina watakapokutana kwenye Robo Fainali ya Kombe la Dunia hapo Jumamosi huko Estadio Nacional Mane Garrincha Mjini Brasilia.
Katika Mechi zao zote 4 walizocheza huko Brazil, Argentina, chini ya Kocha Alejandro Sabella, wameshinda baada ya mchango mkubwa wa Messi.
Hazard amesema kumdhibiti Messi kutawasaidia sana wao kushinda.
Ametamka: “Tunajua wana Mchezaji Bora Duniani kwenye Timu yao, lakini hatuogopi. Tunaweza kushinda. Argentina wamefanya vizuri lakini wanae Mchezaji mmoja ambae ndie huwaletea tofauti katika kila Mechi. Tukimzuia, tuna nafasi, lakini si rahisi.”
Pia, Hazard amesema wana matumaini makubwa ya kuifikia Rekodi ya Timu yao ya Taifa ya Mwaka 1986 ambayo ilifungwa kwenye Nusu Fainali ya Kombe la Dunia.

0 comments: