Ushirikiano wa pamoja unatakiwa 
baina ya wanafunzi, walezi, wazazi, jamii na walimu ili kuweza kujenga, 
kuimarisha na kukuza nidhamu , mwenendo na tabia ya mtoto jambo ambalo 
litaleta mafanikio chanya pamoja na kutatua changamoto za kitaaluma na 
kimazingira.
Hayo yamesemwa  jana  na Mke wa 
Rais Mama Salma Kikwete wakati akiongea na walimu pamoja  na wanafunzi 
wa shule ya Sekondari  Salma Kikwete iliyopo kata ya Kijitonyama wilaya 
ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Mama Kikwete ambaye pia ni 
Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema nidhamu ya
 mwanafunzi siyo tu kumuamkia mwalimu bali pia kujua wajibu wake kama 
vile kuwahi shuleni, kufanya mazoezi ya darasani na kusoma kwa bidii.
“Neno nidhamu lina dhana pana 
kwani linagusa wengi lakini katika mazingira ya leo walengwa wakubwa 
ni mzazi,mlezi au jamii, mwalimu na mwanafunzi. Kazi ya mzazi, mlezi na 
jamii ni kuhimiza na  kufuatilia maendeleo ya mtoto.
Mwalimu kufundisha, kuingia 
darasani kwa wakati  na kujiandaa  na kwa mwanafunzi ni kupokea maarifa 
anayopewa na mwalimu wake na kusoma kwa bidii”, alisema Mama Kikwete.
Kwa upande wa wanafunzi aliwasihi 
kuongeza juhudi katika masomo na kufanya vizuri kwenye mitihani, kwani 
wao na wengine wote wanategemewa na familia, jamii zao na taifa kwa kuwa
 watakuwa wakombozi siku za  baadaye na kumuomba Mwenyezi Mungu awape 
nguvu na ujasiri katika safari yao ndefu ya kufatuta elimu.
Aidha Mama Kikwete aliwapongeza 
walimu wa shule hiyo kwa kazi kubwa wanayoifanya ya uboreshaji wa elimu 
pamoja na kukabiliwa na changamoto kadhaa lakini kadri siku 
zinavyokwenda mbele ndivyo Serikali inavyozidi kutatua changamoto 
mbalimbali zinazowahusu walimu.
Mwenyekiti huyo wa WAMA 
alisisitiza,  “Walimu timizeni wajibu  wenu  kwa kufika kazini mapema, 
kumaliza silabasi kwa wakati, kukamilisha maandalio ya masomo, 
kufundisha kila kipindi bila kukosa, kujua taarifa na udhaifu wa 
wanafunzi wenu na kuwa kiungo kati yenu  na wazazi au walezi hiyo  ndiyo
 nidhamu ya mwalimu na ndiyo ualimu”.
Akisoma taarifa ya shule hiyo 
Mwalimu Elestina Chanafi alisema shule hiyo ilianza mwaka 2007 ikiwa na 
wanafunzi 320, walimu 13 na vyumba vya madarasa sita hivi sasa ina 
wanafunzi 1229, walimu 33 na  vyumba vya madarasa 22. Hadi sasa jumla ya
 wanafunzi 1161 wamehitimu masomo yao tangu walipoanza  kutoa kidato cha
 nne mwaka 2010. 
Mwalimu Chanafi  ambaye ni Mkuu wa
 shule hiyo alisema wamefanikiwa kuchimba kisima cha maji kwa msaada wa 
wakorea, kuunganisha umeme, kununua vifaa mbalimbali vya uchapaji na 
udurushaji, kuboresha mazingira kwa kiwango cha kutia moyo na 
kuweza  kuwavutia wanafunzi ili wajisikie kuwa sehemu ya shule.
Kuanzisha maabara ya muda ambayo 
imewawezesha wanafunzi wa sayansi kufanya mitihani kwa vitendo na 
kuongeza kiwango cha ufaulu kwa masomo hayo na kupata wanafunzi wa 
kujiunga na masomo ya ngazi ya juu kwa idadi nzuri.
“Changamoto zinazotukabili ni 
uchakavu wa baadhi ya vyumba vya madarasa, mmomonyoko mkubwa wa maadili 
ambao unasababisha ugumu katika kudhibiti nidhamu ya wanafunzi, uelewa 
mdogo wa wazazi juu ya mchango wao kwa maendeleo ya wanafunzi, kiwango 
kidogo cha ruzuku toka Serikalini ambacho hakiletwi kwa ukamilifu na 
wakati, ufinyu wa bajeti na ulegevu wa uchangiaji wa ada na michango 
mingine toka kwa wazazi”, alisema Mwalimu Chanafi. 
Naye Mkuu wa wilaya ya Kinondoni 
Jordan Rugimbana alimshukuru Mama Kikwete kwa kupata nafasi ya 
kuitembelea shule hiyo na kumpongeza kwa kazi anayoifanya ya kuinua 
kiwango cha elimu nchini  na kuendeleza fani yake ya ualimu kwa faida ya
 kizazi cha leo na kijacho kwa kuwasomesha watoto zaidi ya 600 hawa ni 
mbali na wanafunzi walioko Shule ya Sekondari WAMA-Nakayama iliyopo 
wilaya ya Rufiji mkoani Pwani.
Mama Kikwete aliichangia shule 
hiyo mifuko 100 ya simenti  ambayo itatumika kuzima mashimo katika 
vyumba vya madarasa ambapo wilaya ya Kinondoni itagharamia mchanga 
pamoja na kumlipa fundi atakayefanya kazi  hiyo. 
Habari Na Anna Nkinda – Maelezo
 






 
 
 
 






0 comments:
Post a Comment