Friday, 13 June 2014

HII NDIYO BAJETI YA SERIKALI KWA MWAKA WA FEDHA 2014/2015





HOTUBA YA MHESHIMIWA WAZIRI WA FEDHA, SAADA MKUYA SALUM (MB) AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA YA FEDHA KWA MWAKA 2014/15
 
UTANGULIZI:
1.       Mheshimiwa Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa hapa Bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali kupokea, kujadili na kupitisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha kwa mwaka 2014/15.
2.       Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniwezesha kuwasilisha hotuba ya bajeti ya Wizara ya mwaka 2014/15. Aidha, natoa shukrani zangu za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuniteua kuwa Waziri wa Fedha. Ninaahidi kwamba nitatekeleza jukumu hili kwa weledi na uadilifu. Vile vile, nawapongeza Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) na Mhe. Adam Kighoma Ali Malima (Mb) kwa kuteuliwa kuwa Naibu Mawaziri wa Wizara ya Fedha. Kadhalika, namshukuru pia aliyekuwa Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Janeth Zebedayo Mbene (Mb) kwa utendaji kazi wake mahiri na tunamuombea Mwenyezi Mungu ampe nguvu na afya njema katika kazi zake mpya Wizara ya Viwanda na Biashara. Nichukue pia fursa hii kumpongeza Bw. Rished M. Bade kwa kuteuliwa kuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania.
3.       Mheshimiwa Spika, napenda kukupongeza wewe mwenyewe, Naibu Spika pamoja na Wenyeviti wa Bunge kwa kuongoza vyema majadiliano ya Bunge la Bajeti.
4.       Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kuishukuru kwa namna ya pekee Kamati ya Kudumu ya Uchumi, Viwanda na Biashara chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Luhaga Joelson Mpina (Mbunge wa Kisesa) na Makamu wake Mhe. Dunstan Luka Kitandula (Mbunge wa Mkinga) kwa maoni, ushauri na mapendekezo waliyoyatoa kwa Wizara wakati wa kuchambua mapendekezo ya Bajeti ya Wizara ya Fedha. Aidha, nachukua nafasi hii kumshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bajeti Mhe. Andrew John Chenge (Mbunge wa Bariadi Magharibi) pamoja na Kamati nzima kwa ushauri wao. Katika uandaaji wa hotuba hii, Wizara imezingatia ushauri na mapendekezo ya Kamati hizo pamoja na ushauri na maoni ya hoja mbalimbali zilizotolewa wakati wa mjadala wa bajeti ya Wizara kwa mwaka 2013/14.
5.       Mheshimiwa Spika, kama unavyofahamu, Wizara ilipata pigo kwa kuondokewa na kiongozi wetu mkuu Marehemu Dkt. William Augustao Mgimwa. Tunawashukuru Viongozi wa Serikali, Waheshimiwa Wabunge, Washirika wa Maendeleo, Taasisi mbalimbali pamoja na wananchi kwa ushirikiano waliotupa kipindi chote cha msiba. Tumeendelea kuenzi misingi imara aliyotujengea marehemu katika kutekeleza majukumu ya Wizara. Aidha, tunapenda kutoa pole kwa ndugu na jamaa kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Chalinze Marehemu Saidi Ramadhani Bwanamdogo. Vile vile, napenda kutoa pole kwa Mheshimiwa Zuberi Zitto Kabwe kwa msiba wa mama yake mzazi aliyefariki tarehe 01 mwezi Juni, 2014. Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi. Amina.
6.       Mheshimiwa Spika, tarehe 27 mwezi Mei 2014, Wizara ya Fedha ilipata pigo tena baada ya kifo cha mke wa Katibu Mkuu - Hazina. Kwa namna ya kipekee naomba nitumie tena fursa hii kutoa pole kwa Dkt. Servacius Likwelile kwa kufiwa na mkewe. Hata hivyo Dr. Likwelile ameendelea kutekeleza majukumu yake katika kipindi chote cha msiba.Wizara inatoa pole kwa ndugu, jamaa na marafiki wa familia yake kwa msiba wa mpendwa wao. Namuomba Mwenyezi Mungu azilaze roho ya marehemu mahali pema peponi. Amina.
7.       Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza, Mhe. Yusuf Salim Hussein Mbunge wa Chambani, Mhe. Godfrey William Mgimwa (Mbunge wa Kalenga) na Mhe. Ridhiwani Jakaya Kikwete (Mbunge wa Chalinze) kwa kuchaguliwa kwao.

Related Posts:

0 comments: