Monday, 16 June 2014

WANANCHI WA LALAMIKIA , WALIA NA UHALIFU UNAOFANYIKA WILAYANI ARUMERU MKOANI ARUSHA

  
Tengeru Arusha 

Wakazi wa Kitongoji cha Bondeni, Kijiji cha Ngurdoto, Kata ya Maji ya chai, Wilayani Arumeru Mkoani Arusha, wameiomba Serikali kuwachukulia hatua kundi la zaidi ya watu 30 wanaofanya uhalifu wa wizi wa kukaba na kubaka.
 
Kundi hilo la vijana kutoka Tengeru na Sing’isi wilayani humo, ambalo ni hatari kama makundi ya mbwa mwitu na panya rodi, huvamia majumbani kwa watu saa 7 hadi saa 9 usiku na kupora vitu ikiwemo fedha, tv na redio.
 
Wakizungumza na waandishi wa habari juzi, baadhi ya wakazi wa eneo hilo ambao waliogoma kutaja majina yao, walidai kuwa kundi hilo linafanya uhalifu kwenye nyumba ambazo hazina wanaume na kuwabaka wanawake.
 
Walidai kuwa mara nyingi, ikifika wakati wa usiku watu hushindwa kutembea kwa hofu ya kukutana na kundi hilo kwani baadhi yao ambao inadaiwa kuwa wana maambukizi ya virusi vya ukimwi hubaka wanawake wa kitongoji hicho.
 
“Tunaiomba Serikali ichukue hatua, kwani ni juzi tu hapa walivamiana nyumbani kwangu na waliua mbwa wangu baada ya kuiba redio, tv na fedha taslimu sh1 milioni,” alisema mmoja kati ya waathirika wa kitongoji hicho.
 
Walisema hivi sasa wanaishi kwa hofu kwani awali kulikuwa na kikundi cha polisi jamii na ulinzi shirikishi na hayo matukio hayakuwepo na Serikali haijachukua hatua au kukemea hali hiyo ambayo haipo kwenye vijiji vingine.
 
Hata hivyo, Mwenyekiti wa kitongoji cha Bondeni Richard Shirima alisema awali kikundi hicho kilikuwa kinasumbua eneo hilo ila hivi sasa hali ni shwari kwani waliweza kuwathibiti vijana wote wanaofanya uhalifu katika kitongoji hicho.
 
“Kama watakuwa wanafanya matukio hivi sasa hao watakuwa wanakuja upya kwani hiyo hali tulishaithibiti ila tutazifanyia kazi hizi taarifa zako ulizotupatia na kuhakikisha hali ya amani inazidi kuwepo eneo hili,” alisema Shirima. 
 
Na Gladness Mushi, Arusha

Related Posts:

0 comments: