Sunday 20 March 2016

Sugu: CCM inatia doa nchi...Dunia Nzima Inaelewa Uchaguzi wa Marudio Zanzibar ni Batili...


WAKATI Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) ikiendelea kusimamia uchaguzi haramu wa marudio visiwani humo, Joseph Mbilinyi, Waziri Kivuli wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo anasema, Serikali ya CCM inatia doa nchi, anaandika Faki Sosi.

Mbilinyi kwa jina maarufu Sugu amesema, Tanzania na dunia nzima inaelewa kuwa marudio ya uchaguzi wa Zanzibar ni batili.

“Na kwa kuwa uchaguzi huu ni batili, watawala yaani Chama cha Mapinduzi kimeingia katika historia ya kipekee duniani kwa kuwanyima haki wananchi wake.”

anasema, matukio mbalimbali yaliyotokea na yanayotokea Zanzibar ikiwemo matumizi ya nguvu, vitisho na hata vitendo vya kikatili dhidi ya wanaosimamia haki, vinaendelea kuitia Serikali ya CCM doa si kwa taifa letu tu pekee bali pia kwa dunia nzima.

Akizungumzia kutekwa kwa Salma Said, Mwandishi wa Habari wa Kampuni ya Mwananchi (MCL) na Makilishi wa Idhaa ya Ujerumani (DW) amesema, tukio hilo limezua maswali na hofu kubwa kwa wananchi, familia yake na wadau hasa wanahabari wa ndani ya nchi na jumuyia za kimataifa.

“Ni dhahiri kuwa, kutekwa kwa Bi. Salma Said kunatokana na kazi yake ya uanahabari na ndio maana ushahidi wa awali ambao umepatikana kwa njia ya ujumbe wa sauti ukiwa na sauti inayoaminika kuwa ni yake, unaelezea wazi kutekwa kwake kunatokana na yeye kuripoti dosari zinazoendelea hasa katika uchaguzi batili wa marudio ya Zanzibar,” amesema na kuongeza;

“Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, inalaani kwa nguvu zote kitendo cha utekaji wa mwanahabari huyu kutokana na kazi yake. Aidha, tunaitaka Serikali kuhakikisha kuwa mama, dada, rafiki na ndugu yetu Bi Salma Said anapatikana akiwa salama.”

Amesema, wataendelea kuamini kuwa, kuchelewa kupatikana kwa Salma na ukimya wa vyombo vya Serikali na Usalama ni matokeo ya uminyaji wa demokrasia kwa wale wasiofanya kazi kwa mashinikizo ya chama tawala.

“Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, itaitisha maandamano makubwa nchini ili kushinikiza upatikanaji wa haraka wa Bi Salma Said lakini pia kupaza sauti kwa ulimwengu kuwa Tanzania si mahali salama kwa wanahabari,” amesema

0 comments: