Wednesday 3 September 2014

Kivuli Cha UKAWA Chamtesa Hamad Rashid


MJUMBE wa Bunge Maalum la Katiba ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati namba 5 ya bunge hilo, Hamad Rashid Mohamed amesema wajumbe wa Bunge hilo wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) wamekosa fursa nzuri kwenye bunge hilo.
Kauli hiyo aliitoa jana ndani ya bunge mjini Dodoma wakati akiwasilisha taarifa ya kamati yake kwa sura 2,3,4 na 5 ya Rasimu ya Katiba:
“Kamati yangu imeomba niwaombe Watanzania wabaki watulivu wasishawishike, wasikilize yaliyo ya kweli, wayapuuze ya uongo,” alisema Hamad.
Alisema kama kuna watu hawakushiriki ni kukosa taaluma ya ndani kabisa na tafsiri sahihi ya vifungu vya Katiba. Aliwaomba wananchi kuikubali Katiba itakayopendekezwa na kutoa maoni yao kwa usahihi pindi itakapowafikia.
Wakati akiendelea kuzungumza Mjumbe wa Bunge hilo, John Cheyo alisimama na kuomba utaratibu wa Mwenyekiti wa Bunge, Samuel Sitta ambapo alimtaka Hamad Rashidi kurejea katika taarifa yake kwa kusoma ibara moja baada ya nyingine:
“Mheshimiwa mwenyekiti kamati ina muda mchache wa kuwasilisha taarifa yake, tukiendelea kwa namna hii hatutapata ibara kwa ibara, tunataka ibara kwa ibara kama waliofanya wale waliosoma mara ya kwanza,” alisema Cheyo.
Hata hivyo, Sitta alimtetea Hamad Rashidi kwa kusema kuwa anatakiwa kusoma taarifa yake kwa kifupi kwa kuwa muda hautatosha endapo atasoma ibara kwa ibara.
Akiwasilisha taarifa ya kamati hiyo Hamad Rashid alisema kuwa katika ibara 206 za sura hizo nne za rasimu ya katiba kamati yake imefuta ibara tano kwa mapendekezo kwamba ibara hizo zitungiwe sheria.
Aliongeza kuwa katika majadiliano kamati yake ilipata theluthi mbili kutoka pande zote mbili za Muungano wakati ikipitisha ibara za rasimu hiyo

CHANZO Gazeti la Majira
Wednesday September 3, 2014
..

0 comments: