Sunday 18 May 2014

MKUU WA MKOA WA RUKWA ENG. STELLA MANYANYA AKAGUA UJENZI WA MIRADI YA MAJI

KATIKA MANISPAA YA SUMBAWANGA, APIGA MARUFUKU UHARIBIFU WA VYANZO VYA MAJI

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Eng. Stella Manyanya (Mb) katikati akitoa maelekezo kwa watendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga na Mkandarasi anaejenga mradi wa maji wa kijiji cha Malonje ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi za Serikali za kufikisha huduma muhimu kwa wananchi. Mradi huo wa maji ambao unaelekea kukamilika umefadhiliwa na benki ya dunia kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania kwa gharama ya Tsh. Milioni 279. Katika maagizo aliyoyatoa ni pamoja na kupiga marufuku shughuli zote za kilimo na ufugaji karibu na vyanzo vya maji kulinda vyanzo hivyo.
Sehemu ya banio la kukingia maji kwenye chanzo cha maji (chemchem) katika kijiji cha Malonje ambalo ni sehemu ya mradi huo, baadhi ya wananchi wameonekana kuendesha shughuli zao za kilimo na ufugaji karibu na chanzo hicho ambapo wamepigwa marufuku kuendeleza shughuli hizo za uharibifu wa chanzo hicho cha maji. 
Bwana Danford Anania Kaimu Injinia wa Maji Manispaa ya Sumbawanga wa pili kulia akitoa maelezo ya tenki la maji lenye ujazo wa lita 45, 000 kwa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Eng. Stella Manyanya. Tenki hilo limejengewa pampu itakayotumia nguvu ya nishati ya jua kusukuma maji katika vijiji vya jirani vya Malonje ikiwa ni sehemu ya mradi wa maji wa Kijiji cha Malonje katika Manispaa ya Sumbawanga.
Banio la kukinga maji kwenye chanzo (chemchem) ikiwa ni sehemu ya ujenzi wa mradi wa Maji katika kijiji cha Mlanda Manispaa ya Sumbawanga ambapo mradi huu utakaotumia zaidi ya Tsh. Milioni 394 unajengwa na mkandarasi Safari General Traders na unategemewa kuhudumia wanachi wa kijiji cha Mlanda. Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Injinia Stella Manyanya alitembelea jumla ya miradi mitano ya Maji katika Manispaa ya Sumbawanga ambayo ni Malonje, Mlanda, Pito, Chilenganya na Kanondo. Aliwataka wakandarasi waharakishe kumaliza kazi walizobakisha ili wanancni waweze kupata huduma hiyo muhimu ya maji. Aidha alikataa kukagua moja ya mradi kwa vile mkandarasi husika amekua akitoa visingizio mbalimbali vya kutokumaliza kazi. 
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Eng. Stella Manyanya akizungumza na wananchi wa kijiji cha Malonje muda mfupi baada ya kukagua mradi wa maji na Zahanati katika kijiji hicho, aliwataka wananchi hao kuwaendeleza watoto wao kielimu na kushirikiana na uongozi wa kijiji katika kuhifadhi mazingira na kulinda vyanzo vya maji. Kulia ni Mkurugenzi wa Manispaa ya Sumbawannga Ndugu William Shimwela.
(Na Hamza Temba – Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Rukwa @rukwareview.blogspot.com)

0 comments: