Monday 18 August 2014

MECHI ZA LIGI KUU BARA, SASA KUCHEZWA USIKU


Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kupitia Bodi ya Ligi, limesema msimu mpya wa Ligi Kuu Bara, ambao unatarajiwa kuanza Septamba 20, utakuwa na mabadiliko makubwa, zikiwemo mechi za usiku.
Ofisa mtendaji wa bodi hiyo, Silas Mwakibinga, amesema wamechukua uamuzi huo kwa ajili ya kuondoa usumbufu wa kuahirishwa kwa mechi bila sababu za msingi, hali ambayo imekuwa ikileta kero kwa wadau wa soka.


Ameongeza kuwa, tayari utaratibu huo umekamilika na mechi hizo zitakuwa katika Uwanja wa Chamazi Complex lakini si Uwanja wa Taifa kutokana na gharama za uendeshaji.

Kwa miaka mingi, kumekuwa na kero ya kuahirishwa kwa mechi kutokana na mgongano wa ratiba, lakini sasa limepatiwa ufumbuzi.

“Msimu huu kuna baadhi ya mechi zitachezwa usiku. Tumeamua kuanzisha kitu kiitwacho ‘match day’, yaani mechi za siku husika. Hatutaki msimu huu na kuendelea kuwepo kero ya kuahirishwa mechi pasipo na sababu za msingi.

“Zitakuwa katika Uwanja wa Chamazi na tayari tumekubaliana kuhusu hilo lakini si kwa upande wa Uwanja wa Taifa, una gharama kubwa za umeme, tofauti na Chamazi,” alifafanua Mwakibinga.

Akifafanua hali ya viwanja, Mwakibinga alisema viwanja vyote vipo tayari kwa matumizi msimu huu, japo Nangwana Sijaona ambao utatumiwa na Ndanda upo katika hatua za mwisho kabisa katika ukarabati, lakini ndiyo utatumika kwa mechi zake.

0 comments: