Saturday 24 October 2015

Sumaye: Ukawa tutaleta katiba ya Wananchi

Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye akiwa jukwaani
Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye akiwa jukwaani
WAZIRI Mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye, amesema serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM) inatumia vibaya madaraka yake, kutokana na katiba iliyopo kuwa mbovu, hivyo Ukawa ikiingia madarakani itahakikisha inapatikana katiba ya Wananchi. Anaandika Moses Mseti, Mwanza … (endelea).
Kauli hiyo imeitoa leo wakati wa mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa shule ya msingi Mbugani Wilaya ya Nyamagana jijini hapa, wakati kufunga kampeni za wagombea ubunge wa jimbo la Nyamagana na Ilemela.
Sumaye amesema kuwa CCM inatumia mwanya wa katiba hiyo kuwakandamiza wananchi kitendo ambacho kimesababisha wananchi kuendelea kuwa watumwa katika nchi yao.
Amesema katiba iliyopo imewanyima uhuru wananchi kuhoji na kuwabana watawala namna ambavyo mapato ya Taifa yanavyotumika na ubadhilifu unaofanywa na Serikali kila kukicha.
“Wabunge wa CCM wao badala ya kuwatetea wananchi ambao ndio mabosi, wenye kazi yao ni kuitetea serikali waendelee kuchakachukua, tukiingia madarakani sisi cha kwanza ni kupata katiba mpya ambayo iatoa nafasi Wananchi kuhoji na kuiwajibisha Serikali.
“Katiba iliyopo sasa hivi inatoa mwanya kwa mahakama kuingilia bunge na hiyo hiyo mahakama bunge haliwezi kuingilia, kwenye ile rasimu ya katiba aliyopeleka Warioba (Jaji Joseph Worioba) ilitaka vitu hivi viwili vijisimamie kwa ukiritimba wa CCM walikakataa,” amesema Sumaye.
Sumaye ambaye alikuwa Mbunge wa Hanang, amesema CCM wamesababisha nchi kuendelea kuwa maskini kutokana na vigogo kuendelea kujilimbikizia mali wao binafsi na kuendelea kuwakumbatia mafisadi.
Amesema serikali imekuwa ikiwakumbatia watu ambao wanaliingiza nchi katika umaskini, lakini wananchi ambao ni maskini imekuwa ikiwabana na kuwafanya kama watumwa katika Taifa lao kwa kukosa mahitaji muhimu ya kijamii.
“Wanapandisha gharama za mafuta ya taa na dizeli kutokana na mafisadi wachache wanao chakachuaji mafuta kukumbatiwa na serikali na mawaziri wake kukuaa kimya na kushindwa kuwadhibiti,” amesema.
Pia Sumaye aliwaomba wananchi kukichagua Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuanzia ngazi ya udiwani, ubunge na nafasi nyeti ya Urais.
Sumaye amesema kuwa endapo watanzania watamchagua, Edward Lowassa, anayegombea kupitia Chadema na kuungwa mkono na Muungano wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ataweza kuondoa umaskini wa wananchi uliodumu tangu uhuru mwaka 1961.

0 comments: