Saturday 23 April 2016

Juma Abdul Jaffar asaini Yanga Mkataba Mpya wa miaka miwili hadi 2018

 
BEKI hodari wa kulia wa kimataifa wa Tanzania, Juma Abdul Jaffar Mnyamani amesaini Mkataba mpya wa miaka miwili kuendelea kuichezea Yanga SC ya Dar es Salaam hadi mwaka 2018.

Habari kutoka ndani ya Yanga zinasema kwamba Abdul alisaini Mkataba huo kabla ya timu hiyo kwenda Misri kucheza na Ahly.

Na hakuna kingine kilichoisukuma Yanga kumsainisha Mkataba mpya beki wake huyo zaidi ya kiwango chake kizuri kwa sasa akionekana kabisa kuwa miongoni mwa wachezaji muhimu kikosini.

Na kwa kusaini Mkataba huo, Juma ataingia kwenye orodha ya wachezaji walioitumikia klabu hiyo kwa muda mrefu.

Juma aliyezaliwa Novemba 10, mwaka 1992
Mwananyamala, Dar es Salaam, alijiunga na Yanga mwaka 2012 akitokea Mtibwa Sugar kwa Mkataba wa miaka miwili, ambao ulipoisha akaongezwa mwingine wa miaka miwili.

Na wakati Mkataba wake wa sasa unaelekea kumalizika mwishoni mwa msimu, inaelezwa tayari Juma Abdul amesaini Mkataba mwingine mpya wa miaka miwili utakaomfanya afikishe miaka sita Jangwani.

0 comments: