Tuesday 12 April 2016

Gari la Serikali Lanaswa Baa Usiku..... Hili ni jipu linahitaji kutumbuliwa

KIKOSI cha Oparesheni Fichua Maovu (OFM) cha Global Publishers, Ijumaa iliyopita kilimnasa dereva wa taasisi ya serikali akirandaranda na gari la serikali usiku na akaishia baa moja ambapo alikutwa akinywa pombe huku akila nyama choma.

OFM wakiwa kwenye hekaheka za kusaka matukio walishuhudia gari hilo (namba tunazihifadhi), likikata mitaa lakini likaishia maeneo ya Mji Mpya kwenye Baa ya Uswaa ambapo saa 4 usiku liliegeshwa na kudumu hapo kwa muda mrefu kinyume na maelekezo ya serikali yanayosema magari yake yote kutembea mwisho saa 12 jioni.

OFM ilimshuhudia dereva wa gari hilo akinywa pombe kinyume na sheria za usalama barabara zinazokataza kutumia kilevi kisha kuendesha chombo cha moto.
“Hii mbaya sana, mambo kama haya mpaka Magufuli (Rais Dk. John Magufuli) aseme? Viongozi wake wapo lakini hawasimamii ipasavyo sheria,” alilalamika mwananchi mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Laudio Kabila.

Alisema maagizo yanapotolewa na rais hugeuka kuwa sheria hivyo haoni sababu polisi wanaosimamia sheria na maagizo ya viongozi tena wa nchi kuacha kusimamia ipasavyo.
0“Polisi ndiyo wanaosimamia sheria na maagizo ya viongozi wa serikali kama vile rais, waziri, mkuu wa mkoa, mkuu wa wilaya na kadhalika. Hili la magari kuzurura hovyo usiku wanalifumbia macho, waache kufanya hivyo,” alishauri Kabila.

Hadi OFM inaondoka kwenye baa hiyo saa sita usiku, ilimuacha dereva huyo akiendelea kupata kinywaji huku akiwa na mwanamke ambaye haikufahamika kama alikuwa mkewe au mpenzi.
Wakati anaingia maradakani mwaka jana, Rais Dk. Magufuli aliagiza magari yote ya serikali kutofanya kazi usiku isipokuwa yale ambayo viongozi wake watakuwa wako kazini.

Alisema magari yote yawe yanaegeshwa sehemu husika serikalini saa 12 jioni isipokuwa kama kuna viongozi au watendaji wa serikali ambao wapo kazini na akaelekeza kwamba yatakayokuwa na shughuli maalum za kiserikali, yawe na vibali.

Agizo kama hilo liliwahi kutolewa na serikali ya awamu ya nne iliyokuwa ikiongozwa na Rais Mstaafu, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete lakini ilikuwa kama nguvu ya soda kwani baadaye lilipuuzwa.
Mbaya zaidi hata jeshi la polisi linalopaswa kusimamia agizo hilo limekuwa likifumbia macho jambo hilo ambalo lilitolewa kwa nia nzuri na kwa faida ya taifa.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, ACP Ulrich Matei (pichani) hakuweza kupatikana mara moja ili kueleza kwa nini hawayakamati magari yanayozurura usiku na kutumika kwa shughuli za starehe kama lilivyokutwa gari hilo mkoani hapa.

Chanzo:Global Publishers

0 comments: