Sunday 11 January 2015

SERIKALI YATOA SHILLINGI MILLIONI 21 MIKOPO KWA AJIRI YA VIJANA

Serikali imewataka vijana kuitumia vyema mikopo wanayopata katika kuteketeza miradi mbalimbali ya kimaendeleo ili kujikwamua kiuchumi.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Msaidizi wa  Ufutiliaji na Tathimini  toka Wizara ya Habari,Vijana,Utamaduni na Michezo Bi.Verdiana Mushi wakati alipotembelea Ofisi ya Halmashauri ya Nzega na kwa ajili ya kukabidhi hundi ya kiasi cha shilingi milioni 21 itakayosaidia kukopesha vikundi vya vijana walioko chini ya Vijana Saccoss Nzega.
“Serikali inaendelea kutekeleza ahadi yake ya kuwasaidia vijana kujikwamua kiuchumi kwa kuwapatia mikopo ambayo itawasaidia kutekeleza miradi mbalimbali ambayo itawaongezea kipato na kuwaondolea umasikini kwani vijana ndiyo nguvu kazi ya nchi” Alisema Bi.Mushi.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nzega Bw. Abrahaman Mndeme ameishukuru serikali kwa kuwapatia mkopo huo vijana wa Nzega kwani kwa kupitia mkopo huo vijana watafaidika sana na pia watachangia kukua kwa pato la Halmashauri na kupunguza vijana wanaoka vijiweni na kushauriana mambo yasiyo na maendeleo katika jamii.
PIX 2
Mkurugenzi wa Halmashauri  ya Nzega Bw. Abrahaman Mndeme akipokea  barua pamoja na hundi zenye jumla kiasi cha shilingi millioni 21 kutoka kwa  Afisa Vijana wa Wizara ya Habari,Vijana,Utamaduni  na Michezo hivi karibuni.
“Uongozi wa Halmashauri kwa kushirikiana na Saccoss ya Vijana Nzega utasimamia gawio la fedha hizo kwa vikundi husika na kuhakikisha miradi iliyoandikwa na vikundi hivyo inatekelezwa, pamoja na kufuatilia urejeshwaji mikopo hiyo kwa wakati ili vikundi vingine viendelee kunufaika na mikopo hiyo inayotolewa na serikali”,alisema Bw.Mndeme
Akitoa hamasa kwa vijana Afisa Vijana kutoka Wizara ya Habari,Vijana,Utamaduni na Michezo Bw.Eliakim Mtawa aliwaasa Vijana kuunda vikundi na kujiunga katika Saccoss za Vijana zilizopo katika halmashauri zao ili waweze kuomba mkopo  utakao wasaidia kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi badala ya kukaa vijiweni.
PIX 3
Afisa Vijana wa Halmashauri ya Nzega Bi.Frida Lwani (watatu  kulia) akifafanua jambo kuhusu maendeleo ya vikundi vya vijana vya  hapo kwa Maafisa kutoka Wizara ya habari,Vijana ,Utamaduni na Michezo walipowatembelea katika ofisi ya halmashauri ya Nzega hivi karibuni.
“Serikali imedhamiria kwa dhati kuwakomboa vijana kiuchumi kwa kutambua changamoto ya ajira iliyopo katika taifa letu  kwa sasa na dunia nzima kwa ujumla”,alisema Bw.Mtawa.
Pamoja na hayo naye Mwenyekiti wa Vijana Saccoss Nzega Bw.Emmanuel Mambo, ameishukuru serikali kwa niaba ya vijana wa Nzega kupitia Wizara ya Habari,Vijana,Utamaduni na Michezo na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana kuwapatia fedha hizo walizoomba kwa ajili ya kufanya miradi mbalimbali ikiwemo ufugaji na kilimo itakayoongeza kipato chao.
 

0 comments: