Saturday, 4 January 2014

WATU 27 WAPOTEZA MAISHA AJALI ZA TRENI MWAKA 2013

Dar es Salaam. Jumla ya watu 27 wamepoteza maisha yao na wengine 27 wamejeruhiwa katika matukio yanayohusisha  ajali za treni zilizotokea nchini mwaka jana.  Kamanda wa Kikosi cha Reli Tanzania, Saada Haji akizungumza na gazeti hili alisema kwamba jumla ya ajali 79 zinazohusisha treni zilitokea mwaka jana katika mikoa tofauti nchini.
Alisema kuwa hata hivyo, ajali nyingi kati ya hizo zimetokana na uzembe, ikiwemo kulewa na kukaa juu ya reli, kuweka ‘headphone’ na kutembea relini na madereva wa magari kukosa umakini wa kufuatilia alama za barabarani kwa kuendesha mwendo kasi hata mahali penye kivuko cha treni.
“Treni linalofanya safari zake ndani ya jiji ndiyo ambalo kwa sasa linahusisha vifo vya watu wengi kwa muda mfupi tangu kuanza kwa safari zake watu 8 wamekufa huku wengine wakijeruhiwa,” alisema Kamanda Haji.
Alisisitiza, ” Hasa katika eneo la Daraja la Buguruni kwa Mnyamani ndiyo eneo ambalo ni hatari, kwani  limekuwa na matukio ya ajali, wananchi wengi hujisahau hukatiza juu ya reli kwa kuwa treni huwa halina breki za papo kwa papo basi vifo  au majeraha makubwa yanayowasababishia ulemavu wa kudumu,” alibainisha.
Akizungumzia kuhusu matukio 285  ya uhalifu alisema kuwa yalitokea katika M ikoa ya Morogoro, Dodoma, Tabora, Mwanza, Kigoma, Mpanda  na Dar es Salaam, ambayo yalitokea  katika maeneo ya reli na ndani ya treli.
“Polisi wa kikosi hiki wamekuwa wakipambana kikamilifu, kuna siku walifanikiwa kukamata mabegi yaliyowekea bangi, ambapo mtuhumiwa alifikishwa mahakamani kujibu mashtaka,” alisema.
Alisema kuwa Polisi hao pia waliwahi kumbaini mhalifu mmoja aliyekuwa amebeba silaha isivyo halali  ndani ya treni ambaye alikurupuka na kuitelekeza silaha hiyo.
Na Beatrice Moses, Mwananchi

0 comments: